Pages


Home » » MWANAFUNZI AJINYONGA BAADA YA KUGUNDULIKA ANA UJAUZITO WA MIEZI MITATU, ALIYEJIFANYA MHUBIRI WA NENO LA MUNGU ABAKA.

MWANAFUNZI AJINYONGA BAADA YA KUGUNDULIKA ANA UJAUZITO WA MIEZI MITATU, ALIYEJIFANYA MHUBIRI WA NENO LA MUNGU ABAKA.

Kamanga na Matukio | 02:53 | 0 comments
Habari na Ezekiel Kamanga, Mbeya.
Mwanafunzi wa Kidato cha Pili katika Shule ya Sekondari Isange na mkazi wa Isanu, Kata ya Isange, Wilaya ya Rungwe Mkoani Mbeya amefariki dunia kwa kujinyonga kwa kutumia kamba ya kufungia ng'ombe mara baada ya kugundulika na ujauzito wa miezi mitatu Mei 11 mwaka huu.

Afisa mtendaji wa Kata hiyo Bwana Anyambege Mwangomo amelitaja jina la marehemu kuwa ni Enitha Ndambo (15), ambaye alikuwa akiishi na bibi yake Bi Emelia Ndenga.

Marehemu alichukua hatua hiyo ya kujinyonga wakati mlezi wake akiwa katika kilabu cha pombe na kamba aliyotumia ilikuwa ndani ya nyumba hiyo waliyokuwa wakiishi.

Polisi walifika eneo la tukio kwa lengo la kuukagua mwili wa marehemu na baada ya kuukagua waliuchukua na kuupeleka katika Zahanati ya Isange kwa ajili ya kufanya upasuaji, ili kuthibitisha kama alikuwa na ujauzito na mara baada ya upasuaji waliwaruhusu wanakijiji kuzika mwili wa marehemu na kiumbe cha mtoto kilichokuwa tumboni.

 Mwili wa marehemu ulifanyiwa uchunguzi na Daktari Kalinga kutoka katika Hospitali ya Serikali ya Makandana iliyopo wilayani humo, na zoezi la upimaji wa kubaini wanafunzi walio na ujauzito ulifanywa na Daktari Anna Mwelevu wa Zahanati ya Isange..

Aidha katika uchunguzi uliofanywa umebaini aliyemsababishia ujauzito ni mwanafunzi wa shule hiyo hiyo Alex Mwaitege, anayesoma kidato cha kwanza.


Wakati huo huo Obelo Mwakilasa (46), mkazi wa Kijiji cha Mwela, Kata ya Kandete wilayani humo ametuhumiwa kumbaka mtoto wa kike mwenye umri wa miaka 14 na kumsababishia maumivu makali katika mwili wake.

Mwenyekiti wa Kijiji hicho Bwana Anania Mwalukasa amesema tukio hilo limetokea Mei 10 mwaka huu, ambapo mtuhumiwa anadaiwa alimuita mtoto huyo kwenye shamba la michai kisha kumfanyia ukatili huo.

Baada ya kukuta anakumbana na mkono wa sheria Mwalikasa alienda kuomba msamaha kwa wazazi wa mtoto huyo ili wamsamehe, ombi ambalo lilipokelewa na kusamehewa.

Aidha imedaiwa kuwa mtuhumiwa huyo alifika kijijini hapo kwa mbinu ya kuhubiri neno la Mungu.

Kwa upande wake Mwenyekiti Bwana Mwalukasa ameonekana kukasirishwa na kitendo cha wazazi hao kusameheana nyumbani na kudai kuwa tabia hiyo ikiendekezwa itasababisha kuendelea kwa vitendo viovu kijijini hapo.

Madhara hayo yaliyosababishwa na Bwana Mwakilasa kwa mtoto huyo hayajaweza kufahamika kutokana na wazazi kutompeleka mtoto wao kufanyiwa uchunguzi katika Kituo chochote cha huduma ya Afya(Zahanati/Kituo cha afya/Hospitali).

Hata hivyo vitendo hivyo vya ubakaji wilayani humo vimeota mizizi kutokana na baadhi ya wazazi kufumbia macho kwa kupewa pesa.
Share this article :

0 comments:

 
Support : Creating Website | Greyson Salufu Template | Chimbuko Letu Inc
Copyright © 2011. Kamanga na Matukio - All Rights Reserved
Template Modify by Chimbuko Letu Inc
Proudly powered by Blogger