Pages


(CCM) Wilaya ya Chunya mkoani Mbeya kimeanza kuwajengea uwezo viongozi wake.

Chimbuko Letu | 10:20 | 0 comments
Na Ezekiel Kamanga, Kyela.
 
CHAMA cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Chunya mkoani Mbeya kimeanza kuwajengea uwezo viongozi wake kuanzia ngazi ya kitongoji, kijiji, matawi na Kata ili kusaidia utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi mkuu uliopita.
 
Akizungumza na Kituo hiki, Katibu wa Siasa, Itikadi na Uenezi wa CCM Wilaya ya Kyela, Richard Kilumbo alisema zoezi hilo lilianza mwezi machi na linatarajiwa kukamilika Aprili mwaka huu.
 
Alisema lengo la mafunzo kwa viongozi wa matawi, vitongoji, vijiji na Kata wa Chama cha mapinduzi ni kuwajengea uwezo juu ya namna ya kusaidiana na uongozi wa serikali katika kutatua kero mbali mbali katika jamii pamoja na kusaidia utekelezaji wa ahadi zilizotolewa kwenye uchaguzi mkuu 2015.
 
Alisema Wilaya hiyo yenye vitongoji zaidi ya 300, vijiji 101 na Kata 37 itasaidia viongozi hao kuwa kiungo kizuri kati ya Chama na Serikali ili kurahisisha upatikanaji wa huduma kwa jamii.
 
“Lengo letu tunataka kuwe na mahusiano mazuri baina ya wananchi, Serikali iliyopo madarakani na Chama kuanzia ngazi ya chini ya tawi kwani hili litasaidia sana kusukuma gurudumu la maendeleo ili kwendana na kasi ya Rais” alisema Katibu huyo.
 
Aliongeza kuwa endapo viongozi hao watakuwa na maelewano mazuri na uongozi wa Halmashauri kwa kushirikiana na Madiwani waliopo itasaidia kuisimamia serikali katika utekelezaji wa miradi mbali mbali katika maeneo yao.
 
Alisema mara nyingi viongozi wa serikali hawana mahusiano mazuri na uongozi wa chama katika ngazi za chini jambo linalosababisha kutokuwa na maendeleo pamoja na miradi mbali mbali kukwama.
 
Katibu huyo alisema lengo linguine la mafunzo hayo ambayo wahusika hufuatwa kwenye maeneo yao ni kuondoa makando kando ya uchaguzi uliopita kwa kile alichodai bado kuna mgawanyiko baina ya wanachama na viongozi.
 
“pia ikumbukwe kuwa katika kipindi cha uchaguzi kulikuwa na matabaka ambayo sio kweli kuwa yameisha licha ya kuhubiriwa kwenye majukwaa lakini tunachofanya sasa ni kuelezana madhara ya mgawanyiko katika shughuli za maendeleo kwa jamii tunayoiongoza” alisema Katibu.

Zaidi ya shilingi 25.9 milioni zimeahidiwa ili kufanikisha ujenzi wa chumba cha kuhifadhia maiti.

Chimbuko Letu | 10:19 | 0 comments
Na Ezekiel Kamanga,Chunya.

Zaidi ya shilingi 25.9 milioni zimeahidiwa kutolewa na wadau mbalimbali wa maendeleo katika halmashauri ya wilaya ya Chunya ili kufanikisha ujenzi wa chumba cha kuhifadhia maiti(mochwali) katika hospitali ya wilya ya chunya ili kuhakikisha changamoto hiyo inatoka hospitalini hapo.

Wadau hao wa  maendeleo katika halmshauri ya wilaya ya Chunya wametoa ahadi hizo katika kikao  na mkuu wa wilaya ya Chunya  Elias John Tarimo kujadili ujenzi wa Chumba cha kuhifadhia maiti(Mochwali) katika hospitali ya wilaya ya chunya ili kuhakikisha miili ya marehemu inasaminiwa.

Tarimo alisema ameamua kuwaita wadau wa maendeleo katika halmshauri ya wilaya ya chunya ili kuwahamasisha katika suala zima la kufanikisha  mara moja  ujenzi wa chumba cha kuhifadhia maiti katika hospitali ya wilaya kutokana na umuhimu wake kwani ni aibu kwa wilaya kongwe kama Chunya kukosa sehemu ya kuhifadhi maiti.

Alisema lazima watambue kila mtu ni marehemu mtajiwa hivyo ni wajibu wa kila mmoja kuona umuhimu wa kuchangia fedha ili kuhakikisha halmashauri inapata jengo la kuhifadhia maiti.

Aidha wadau waliohudhuria kikao hicho   kwa kuona umuhimu wa jambo hilo wameweza kujitoa kwa  kupeleka mawe na mchanga lori 11,mifuko ya cement 229,na kutengeneza mirango na madirisha kwenye jengo la hilo kwaajili ya kuanza ujenzi mara moja  na kuazimia kwamba ifikapo desemba mwaka huu wawe wamekamilisha ujezi wa jengo la kuhifadhia maiti katika hospitali hiyo.

Mbali na kutoa michango mbalimbali waliweza kuunda kamati itakayokuwa ikifwatilia kwa ukaribu ujenzi wa jengo la hilo la kuhifadhia maiti hospitalini hapo ili kuhakikisha kasi hiyo inaendana na makubaliano hayo.

Wachimbaji wa Madini watakiwa kutumia Teknolojia za kisasa ili kuepukana na hasara wanazozipata katika uzalishaji.

Chimbuko Letu | 10:18 | 0 comments
Na Ezekiel Kamanga,Chunya.

Chama cha wachimba madini mkoani Mbeya tawi la Chunya(Mberema)wametakiwa kuachana na kuchimba madini kwa mazoea badala yake watumie Teknolojia za kisasa ili kuepukana na hasara wanazozipata katika uzalishaji.

Haya yameelezwa na mawakala wa  Jiolojia Tanzania(GST) kutoka Dodoma  katika kikao cha chama cha wahimba madini tawi la Chunya (mberema) Kilichokuwa kikiongozwa na mwenyekiti wa wachimba madini mkoa wa Mbeya Leonard Manyesha,wakati wataalamu hao wakitoa elimu juu utafiti wa miamba  kwa kutumia vifaa vya kisasa ili kubaini uwepo wa madini  wanayoyatafuta.

Wakitoa mada kwa wachimbaji madini kwa njia ya kisansi mjiolojia  Alphoncce Michael na mjiofizikia Octavian Minja walisema utafutaji wa madini kwa njia ya jiolojia hutumika kuanisha miamba na madini kwenye eneo husika na  kupata taarifa kwa haraka zaidi na hupunguza gharama za uendeshaji kwa kuokoa muda na kujua uwepo wa madini au laa.

Walisema baada ya kufanya tafiti mchimbaji anaweza kujua ni nini afanye ili aweze kupata kile anachokihitaji kwani wamedai kuwa njia za asili za kutazama kwa macho kwa kuangalia aina ya udongo zinachua muda mrefu na hutumia nguvu nyingi na gharama huwa kubwa bila kujua kama anchokitafuta atakipa ipasavyo.

Aidha wachimbaji waliohudhulia kikao hicho walisema waliwashukuru mawakala hao wa jiolijia kwa kuwaletea  elimu hiyo ya uchimbaji wa kisasa na kuomba ofisi ya madini kwa kushirikiana na  halmashauri ya wilaya ya chunya ieweze kuwasaidia  kuhakikisha  mitambo hiyo ya  kufanyiwa utafiti inawafikia wachimbaji kwenye maeneo yao ya kazi ili kuhakikisha wanafanya kazi kwa manufaa.

WANAWAKE WATAKIWA KUJIHUSISHA NA UJASIRIAMALI

Chimbuko Letu | 10:16 | 0 comments
Na Ezekiel Kamanga,Chunya.

Wanawake wa halmashauri ya wilaya ya Chunya Mkoani Mbeya wametakiwa kujihusisha na ujasirimali ili waweze kufikia malengo ya hamsini kwa hamsini na kuachana na dhana  ya kutegemea  wanaume pekee kama ndio wazalishaji wakuu katika familia.

Haya yameelezwa na mwenyekiti wa UWT wilaya ya Chunya Mboka Konzo wakati akizungumza na mwandishi wa habari kuhusiana na mwamko wa wanawake wa halmashauri ya Chunya kujihusisha na shughuli za ujasirimali ukilinganisha na miaka ya nyuma.

Konzo alisema mwamko wa wanawake kwa halmashauri ya Chunya kwasasa umekuwa mkubwa ukilinganisha  miaka ya nyuma  walikuwa wakitegemea wanaume kwa kila kitu huku wao wakibaki nyumbani waletewe chochote lakini kwasasa wanawake wanajishughulisha na  ujasirimali mdogo mdogo kama kuuza mboga mboga,mamamntilie na hata kuzungusha matunda.

Aliendelea kueleza kuwa mbali na kuwa na kasi ya kujihusisha na ujasiriamali wanawake wamekuwa wakiungana katika vikundi vya kukopa na kurejesha (upatu)ambavyo vimekuwa vikiwawezesha wanawake wengi kujikwamua kiuchumi.

Aidha wakizungumzia suala la ujasiliamali baadhi ya wajasirimali wadogo wadogo Esta George na Rehema Charles wanaojihusisha na uuzaji wa matunda katika stend ya chunya mjini walisema kuwa kwasasa wanajitambua na kwamba wameamua kujihusisha na ujasiriamali kama njia ya kusaidiana katika majukumu.

Ambapo waliongeza kuwa licha ya kusaidiana katika majukumu wanafanya hivyo ili kesho na kesho kutwa mwanaume asipokuwepo waweze kusimama wenyewe na kuendesha familia zao bila kuteteleza kwani wamekuwa wakiona wanawake wenzao ambao wamekuwa wakitegemea wanaume jinsi wanavyohangaika wanapoondokewa na waume zao.

Mkuu wa Mkoa wa Songwe Luten Mstaafu Chiku Galawa ameanza ziara ya kutembelea Wilaya zote tano za Mkoa huo.

Chimbuko Letu | 09:24 | 0 comments

Chiku Gallawa
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Joseph Magufuli katika picha ya pamoja na Makamu wa Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu Mhe Kassim Majaliwa na Luteni Mstaafu Chiku Gallawa baada ya kumuapisha kuwa mkuu wa mkoa mpya wa Songwe Ikulu jijini Dar es salaam leo Machi 28, 2016.
Na Ezekiel Kamanga, Songwe

Mkuu wa Mkoa wa Songwe Luten Mstaafu Chiku Galawa ameanza ziara ya kutembelea Wilaya zote tano za Mbozi Songwe,Ileje,Momba na Songwe ambazo zinaunda Mkoa wa Songwe ili kujitambulisha kwa wananchi na kupokea changamoto mbalimbali zinazozikabili wilaya hizo.

Galawa ameanza ziara katika Wilaya ya Songwe ambapo alipokelewa katika Kijiji cha Kaloleni Kata ya Mkwajuni na Vijana waendesha Bodaboda walioambatana na Mbunge wa Jimbo la Songwe Philip Mulugo ambaye ni mlezi wa Vikundi mbalimbali vya waendesha pikipiki Wilaya ya Songwe.

Mkuu wa Mkoa Chiku Galawa alipokea changamoto mbalimbali za Jimbo la Songwe kutoka kwa Mbunge wa Jimbo hilo ikiwa ni pamoja maji,barabara,umeme na Afya.

Mulugo amesema kuwa wilaya hiyo mpya ina eneo la kutosha kujenga nyumba za watumishi wa wilaya hiyo na ofisi mbalimbali pia Asasi ikiwa ni pamoja na ujenzi wa Benki ya NMB ili kuwaondolea adha wakazi wa Mkwajuni kutokana na kutokuwepo kwa Taasisi za kifedha.

Kwa upande wa Mkuu wa Mkoa kabla ya kuwawahutubia wananchi katika uwanja wa michezo wa Mkwajuni alivikwa uchifu na wazee wa kimila wa kabila la Kibungu wakiongezwa na Chifu Kazumba ambaye pia alimkabidhi mbuzi mnyama kama ishara ya upendo na ukaribisho wilayani humo.

Akiwahutubia mamia ya wakazi wa Mkwajuni Galawa amweshukuru wakazi wa Mkwajuni kwa maaribisho mazuri na kusema kuwa changamoto zilizopo katika Mkoa wake mpya zitumikke kama fursa ya kuleta maendeleo katika wilaya hiyo na Mkoa kwa ujumla.

Amesema Wilaya ya Songwe ina ardhi nzuri,Ziwa Rukwa na madini mbalimbali ambayo yatakuwa chachu ya maendeleo kama Dhahabu,makaa ya mawe na madini adimu duniani yanayotumika kutengezea vifaa vya elekroniki ambayo yanapatikana katika Kata ya Ngwala.

Galawa ataendelea na ziara yake katika wilaya za Mbozi Momba,Ileje na Mbozi ambapo atakuwa na kazi ya kupokea kero kutoka kwa wananchi na kuzipatia ufumbuzi ili kuleta maendeleo katika Mkoa wa Songwe.

Waziri Nape Nnauye amesema sekta ya habari nchini inakabiliwa na changamoto kubwa.

Chimbuko Letu | 09:00 | 0 comments
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mh. Nape Nnauye akizungumza na wadau wa Habari,Michezo na sanaa Mkoa wa Mbeya (hawapo pichani)katika ukumbi wa Mikutano wa Mkapa jijini Mbeya April 2 ,2016 .(Picha Keneth Ngelesi)


Na Ezekiel Kamanga, Mbeya.

Waziri wa Habari, Utamaduni Sanaa na Michezo, Nape Nnauye amesema sekta ya habari nchini inakabiliwa na changamoto kubwa kwa waandishi wake kushindwa kufanya utafiti na kwenda kufanya kazi kwenye matukio.

Waziri Nape aliyasema hayo  alipokuwa akizungumza na wanachama wa Chama cha Waandishi wa habari za Utalii na Uwekezaji Tanzania(TAJATI) alipotembelea makao makuu ya chama hicho jijini Mbeya.

Alisema changamoto ya waandishi kushindwa kwenda kupata habari kwenye matukio na kutokufanya utafiti wa kutosha hupelekea habari nyingi kupikwa na kukosa weledi pamoja na kutokuwa na manufaa kwa jamii.

“Habari nyingi huandikwa kutoka habari maelezo basi lakini mwandishi akifanya utafiti na kwenda field kutasaidia kuja na habari nzuri yenye manufaa kwa jamii” alisema Nape.


Waziri Nape alisema changamoto hiyo inaweza kuondolewa endapo mswada wa sheria ya habari uliorekebishwa utapitishwa bungeni baada ya kupitiwa upya. 

Alisema uboreshaji wa mswada wa sheria ya huduma ya vyombo vya habari unaondoa kipengele cha sheria kandamizi  ya kufungia magazeti hukosesha ajira kwa watu wengi badala ya kumwajibisha mhusika mwenyewe ili afanye kazi kwa weledi.

Waziri Nape alipongeza ubunifu uliofanywa na waandishi wa habari kwa kuunda Chama ambacho kitasaidia kuwainua waandishi wa habari ili kuandika habari zenye weledi na faida kwa jamii.

“Niwapongeze TAJATI kwa kuanzisha chama hiki, hiyo ni ndoto yangu mimi kuona sisi waandishi tunafanya kazi mbele zaidi ya kuandika ni jambo zuri kwa mwandishi kuspesholaizi kitu kimoja” alisema Nape.

Alisema kupitia TAJATI itasaidia kuwepo kwa uwajibikaji kwa Serikali kuhusiana na maswala ya utalii na uwekezaji kwani kila kitakachoandikwa kimekuwa kimefanyiwa utafiti ambapo pia sekta hizo zitaimarika vizuri.

Aidha alitoa wito kwa uongozi wa Tajati kuhakikisha Chama hicho kinafungua matawi katika mikoa mingine ili kukifanya kubeba taswira ya kitaifa zaidi kuliko kuwepo katika Mkoa mmoja.

Awali akimkaribisha Waziri, Mwenyekiti wa TAJATI Ulimboka Mwakilili alisema chama kina mikakati mikubwa ya kujitangaza mikoani ambapo kwa kuanzia tayari mikoa mitano ya Kanda ya Nyanda za juu kusini imepata wawakilishi.

Alisema baada ya usajili wanachama kama timu wameshafanya kazi ya kutambua vivutio vya utalii na kutembelea viwanda vinavyofanya kazi na vilivyokufa ili kujua sababu iliyopelekea kushindwa kuendelea kuzalisha.

“Nikupongeze Waziri kwa kuwa kiongozi wa kwanza wa serikali kufika ofisini kwetu, hii ni ofisi ya kitaifa ambayo inaunga mkono hoja yako ya kutaka makao makuu kuondoka jijini Dar es Salaamnasi tumefanya hivyo, pia tayari tumeanza kufuatilia viwanda ili kuendana na sera ya serikali ya awamu ya tano kuwa na uchumi wa viwanda” alisema Mwakilili.

Mwenyekiti ashikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoani Mbeya kwa tuhuma kufuja mali.

Chimbuko Letu | 08:47 | 0 comments
Na Ezekiel Kamanga.
Jeshi la Polisi Mkoani Mbeya linawashikilia Mwenyekiti wa Kitongoji cha Nsalala Stephano Mshani(CHADEMA)na Mtendaji Lwitiko Mwaibindi kwa tuhuma za kuuza ardhi ya Kijiji na fedha kujimilikisha kwenye akaunti mbili za Mwenyekiti.

Tukio hilo limetokea katika mkutano wa hadhara baada ya wananchi kuwatuhumu viongozi hao kwa kuuza mali ya umma kisha kujimilikisha jumla ya shilingi milioni nane laki sita na elfu hamsini bila ridhaa ya wananchi wa kitongoji cha Nsalala.

Katika mkutano iliofanyika machi 26 mwaka huu wananchi hao walimwandikia Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya Upendo Atu Sanga wakitaka kuundwa kwa Tume ya uchunguzi ili kubaini fedha zinazodaiwa kuhodhiwa na viongozi hao bila ridhaa ya wananchi.

Baada ya kupokea malalamiko hayo Mkurugenzi alituma Tume ya uchunguzi ambapo ilibaini tuhuma mbalimbali dhidi ya viongozi hao na kuyasoma maagizo mbele ya mkutano wa hadhara uliofanyika April mosi mwaka huu katika uwanja wa shule ya msingi Nsalala.

Barua hiyo kutoka kwa Mkurugenzi ilisomwa mbele ya wananchi na Mwanasheria wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya Prosper Msivala amabayo ilibaini kuwa :-

(a)Mwenyekiti Stephano Mshani anatuhumiwa kwa makosa yafuatayo:-
(i)Kushiriki kuuza mali ya Umma kinyume cha sheria ya manunuzi ya Umma ya mwaka 2011.
(ii)Kutunza fedha zilizotokana na mauzo hayo kwenye akaunti zake binafsi mbili zilizopo Benki ya NMB Mbalizi Road zenya namba 6251000804 na 62510009 zote zikimilikiwa na Stephano Mshani.

(b)Mtendaji wa Kitongoji(Lwitiko Mwaibindi)anatuhumiwa kwa:-
(i)Matumizi mabaya ya madaraka kwa kushindwa kusimamia Kitongoji na kuwapotosha wananchi.
(ii)Kughushi nyaraka na mikhutasari ya vikao
(iii)Kukodisha eneo la maziko kwa shughuli za kilimo bila kufuata taratibu.
(iv)Kuuza mali ya Umma kinyume na taratibu ya manunuzi ya Umma ya mwaka 2011.
(v)Matumizi mabaya ya muhuri ambao siyo halali.
(vi)Kumdanganya Mwajiri kwa kuficha ardhi ya Mamlaka na kutokabidhi kwa mamlaka.

Hivyo kutokana na makosa hayo Mkurugennzi Mtendaji wa Wilaya ameagiza mosi eneo lililouzwa kurudishwa mara moja kwenye Maml;aka ya Mji mdogo kuanzia April mosi mwaka huu.

Pili Mtendaji wa Kitongoji(Lwitiko Mwaibindi)anasimamishwa kazi kuanzia April mosi mwaka huu ili kupisha uchunguzi wa tuhuma zinazomkabili.

Tatu Polisi na vyombo vya Dola vimchukulie hatua stahiki Mwenyekiti wa Kitongoji cha Nsalala Stephano Mshani.

Uchunguzi umebaini kabla ya mkutano huo viongozi hao walikuwa na taarifa mbili za mapato na matumizi yenye kuonesha kuwa baadhi ya wadau walichanga jumla ya shilingi milioni tatu laki nane arobaini na tatu elfu(3,843,000/=) ambazo zilitumika zote kununua vifaa vya ujenzi,malipo ya mafundi na kusafirishia vifaa vya ujenzi kwa ajili ya shule ya msingi Nsalala.

Taarifa ya mauzo ya shamba shilingi 8,650,000/= ambazo zinaonesha kununulia vifaa vya ujenzi fedha ambazo zilitunzwa kwenye akaunti binafsi za Stephano Mshani kuwa akaunti ya Kitongoji ilikuwa haifanyi kazi kwa muda mrefu.

Baada ya Mwanasheria kuisoma barua hiyo kutoka kwa Mkurugenzi Stephano Mshani na Lwitiko Mwaibindi walichukuliwa na Jeshi la Polisi kwa mahojiano na Diwani wa Kata ya Nsalala Kissman Ngomale alifunga mkutano kwa kuwataka wananchi kuwa wavumilivu ili kusubiri hatua stahiki dhidi ya viongozi hao ikiwa ni pamoja na kufikishwa mahakamani.

Wananchi mkoani Songwe wametakiwa kuzitumia fursa ili kujipatia maendeleo.

Chimbuko Letu | 08:40 | 0 comments
 Luteni Mstaafu Chiku Galawa Mkuu Mpya wa Mkoa wa Songwe (Mkoa Mpya).
Wananchi mkoani Songwe wametakiwa kuzitumia fursa zinazotokana na changamoto zinazowakabili kwa  kufanya kazi kwa bidii ili kujipatia maendeleo na kutimiza wajibu katika majukumu yao ya kila siku.


Rai hiyo ilitolewa jana na Mkuu wa Mkoa wa Songwe (zamani Mbeya) Luteni Mstaafu Chiku Galawa wakati wa hafla ya makabidhiano ya ofisi kati yake na aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Abbas Kandoro iliyofanyika katika makao makuu ya Mkoa wa Songwe yaliyopo Vwawa wilayani Mbozi.


Galawa alisema uwepo wa changamoto mbali mbali katika mkoa huo ndiyo iwe chachu kwa wananchi kutumia fursa hiyo kwa kufanya kazi kwa bidii na ushirikiano ili waweze kuziondoa kwa pamoja na kuufanya mkoa huo kusonga mbele kimaendeleo licha ya kuwa Mkoa mchanga.


“Pamoja na Mkoa wetu kuwa mchanga napenda kuwaambia kuwa tuzitumie changamoto zilizopo kama fursa ya kupata maendeleo na kinachotakiwa ni kila mmoja wetu kuwajibika katika nafasi yake kwani kwa kufanya hivyo wengine watakuja kujifunza Songwe ingawa ni Mkoa Mchanga” alisema Galawa.


Aliongeza kuwa wananchi wanatakiwa kuwa kitu kimoja kwa kufanya kazi kwa mshikamano ili kuenzi umoja na utulivu kwa kila mtu kutii sheria bila shuruti kwa kuepuka kudai haki kwa vurugu kwani athari zake ni kubwa na kuzolotesha shughuli za uzalishaji mali kutokana na kupunguza rasilimali watu, muda na uharibifu wa mali za umma.


Awali akizungumza katika makabidhiano hayo, Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Mstaafu, Abbasi Kandoro alisema ni vema Mkuu wa Mkoa wa Songwe akajikita katika kutatua changamoto za Wananchi kwani wengi wao ni wachapa kazi ambao hawasubiri kutumwa kwenye shughuli za uzalishaji mali hususani kilimo.


Alisema awali Mkoa wa Mbeya ulikuwa mkubwa jambo lililochangia Changamoto nyingi kushindwa kutatuliwa kwa wakati lakini sasa Mkoa wa Mbeya unabaki na kilomita za mraba 34606 huku Mkoa mpya wa Songwe ukibaki na kilomita za mraba 29011 ukiwa na Wilaya 4, Halmashauri 5, Tarafa 12, Kata 74, vijiji 307 na mitaa 71.


Alisema Wananchi wa Songwe wanakabiliwa na changamoto kubwa ya uvunjifu wa amani unaotokana na kudai haki pasipo kufuata sheria jambo linalopelekea kuchoma barabara na kuharibu mali hali inayojitokeza zaidi Tunduma, Vwawa na Mlowo.


Alisema tatizo linguine ambao Mkuu wa Mkoa anapaswa kuliangalia kwa ukaribu akishirikiana na viongozi wa mila nadini ni pamoja na  mauaji ya kishirikina pamoja na kujichukulia sheria mkononi hali inayosababishwa na imani za kishirikina, ulevi, wivu wa kimapenzi na ujambazi.


Wakati huo huo Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Mbeya, Nyasebwa Chimagu alisema baada ya makabidhiano ya ofisi kazi inapaswa kuanza moja kwa moja ambapo baadhi ya watumishi walipewa uhamisho wa muda ili kuendelea na kazai katika Mkoa mpya wa Songwe.


Nyasebwa aliwataja watumishi hao kuwa ni pamoja na Dereva wa Mkuu wa Mkoa Samson Lyimo, Karani wa Mkuu wa Mkoa, Jesca Ndaga, Katibu wa Mkuu wa Mkoa, Devotha Chacha na Kaimu Katibu tawala Msaidizi(Utawala) ambaye alikuwa Katibu tawala Wilaya ya Kyela.

UHAMIAJI HARAMU, UINGIZWAJI WA POMBE HARAMU NA DAWA ZA KULEVYA WAZIKUTANISHA WILAYA MBILI ZA TANZANIA NA MALAWI KUJADILI SULUHISHO.

Chimbuko Letu | 10:25 | 0 comments
 Mkuu wa Wilaya ya Kalonga, Nchini Malawi Rosemary Kalonga na Mkuu wa Wilaya ya Kyela Dk Thea Ntara.
 Maafisa Usalama kutoka Wilaya ya Kyela nchini Tanzania.
 Maafisa Usalama kutoka Wilaya ya Karonga nchini Malawi.
 Maafisa Mifugo kutoka Wilaya za Kyela na Karonga


Kikao cha ujirani mwema baina ya Wilaya ya Kyela nchini Tanzania na Karonga nchi ya Malawi kimefanyika katika ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kyela kwa ajili ya kujadili changamoto zinazozikabili Wilaya hizo.
Wilaya ya Kyela iliwakilishwa na Mkuu wa Wilaya Dakta Thea Ntara na kwa upande wa Wilaya ya Karonga iliwakilishwa na Rosemary Moyo na baadhi ya changamoto kubwa zinazozikabili Wilaya hizo ni pamoja na wahamiaji haramu,madawa ya kulevya,pombe kali na wizi wa pikipiki.
Baadhi ya wajumbe kutoka pande zote mbili wamesema kuwa tatizo la wahamiaji haramu kutoka nchi za Ethiopia,Somalia,Congo,Burundi,Rwanda na Nigeria kunachangiwa na ukoefu wa umakini kutoka mipaka ya kaskazini ambapo huwaacha wahamiaji hao kuingia kiholela.
Sababu nyingine inachangiwa na baadhi ya watumishi wa umma wa pande hizo mbili  wa kutodhibiti vitendo hivyo kutokana wa baadhi ya wahamiaji kutumia pesa pindi wanapokamatwa na baadhi ya maafisa usalama wasio waaminifu.
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Karonga Rosemary Moyo amesema kuwa Watanzania na Wamalawi ni ndugu wa damu ambao wametenganishwa na wakoloni kwa njia ya mpaka wa mto Songwe kwani mpaka sasa raia wa mpakani huvuka kutembeleana kila siku na wengi wao wameoleana kutoka pande hizo mbili.
Hata hivyo kutokana na tatizo hilo kubwa kwa nchi hizo Serkali zote huingia gharama kubwa kuwatunza na kuwasafirisha wahamiaji haramu  kuwarejesha nchi walizotoka.
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Kyela Dakta Thea Ntara amesema wilaya ya Kyela imeimarisha ulinzi mpakani kwa kushirikiana na wananchi ndiyo maana wamefanikiwa kukamata wahamiaji wengi haramu waliojaribu kuvuka mpaka kupitia wilaya hiyo hivyo juhudi kubwa zifanyike ili kuhakikisha tatizo hilo linakomeshwa kabisa.
Hata hivyo elimu itolewe kwa raia wa pande zote mbili ili watu wanaowatilia shaka watolewe taarifa katika vyombo vya ulinzi na usalama vya nchi hizo.

PICHA 12 ZA UBOMOAJI WA VILABU VYA POMBE KYELA ILI KUTOKOMEZA UGONJWA WA KIPINDUPINDU ZOEZI LILILOENDESHWA NA MKUU WA WILAYA HIYO DK THEA NTARA.

Chimbuko Letu | 10:24 | 0 comments

KIPINDUPINDU;- Watu 17 wakamatwa kwa kukosa vyoo na uchafu wa mazingira Mkoani Mbeya.

Chimbuko Letu | 08:58 | 0 comments


 Mkuu wa Wilaya ya Kalonga, Nchini Malawi Rosemary Kalonga na Mkuu wa Wilaya ya Kyela Dk Thea Ntara.

Na Ezekiel Kamanga.
Watu 17 wakazi wa Kijiji cha Lusungo Kata ya Lusungo Wilaya ya Kyela Mkoani Mbeya wamekamatwa kwa kutokuwa na vyoo na uchafu wa mazingira hivyo kuzorotesha juhudi za kupambana na ugonjwa wa kipindupindu Wilayani humo.


Ugonjwa huo umedumu kwa kipindi cha miezi mitatu sasa na Kata ya Lusungo na Ndobo ndizo pekee bado zina wagonjwa wa kipindupindu hali iliyomfanya Mkuu wa Wilaya ya Kyela Dakta Thea Ntara kupiga kambi Kata ya Lusungo ili kufanya ukaguzi wa vyoo na usafi wa mazingira.


Hata hivyo juhudi za Mkuu wa Wilaya zinakwamishwa na Diwani wa Kata ya Lusungo Veronica Kanyanyila na Mwenyekiti wa Kijiji Zawadi Lugano Mwangojola ambao wamekuwa wakidai ugonjwa huo umesababishwa na imani za kishirikina na si uchafu au ukosefu wa vyoo.


Katika oparesheni hiyo maalumu iliyofanywa na Mkuu wa Wilaya aliyeambatana na Maafisa wa Afya pia iliyakumba maeneo mbalimbali kama Kata ya Ikama na Kijiji cha Tenende ambapo alilazimika kuvunja Kilabu cha pombe Kata ya Ikama baada ya kuwakuta wakazi wa eneo hilo wakinywa pombe za kienyeji katika mazingira machafu.


Mbali ya ukaguzi huo pia Mkuu wa Wilaya alishuhudia baadhi ya wananchi wakinywa pombe ya moshi na pombe zilizopigwa marufuku kutoka nchi jirani na kulazimika kuwakamata wahusika ambao wamefikishwa kituo kikuu cha Polisi Wilaya ambapo pindi uchunguzi utakapokamilika watafikishwa mahakamani.


Dakta Thea aliteketeza sindano zinazodhaniwa kutumika kwa ajili ya kujidunga wakati wa matumizi ya madawa ya kulevya katika Kata ya Ikama na ametoa agizo la kuwasaka wauzaji wa madawa hayo na wanaouza pombe zilizopigwa marufuku kutoka nchi jirani.


Kwa upande wake Afisa Afya Geophrey Baroshi amesema kuwa zoezi hilo ni endelevu na watahakikisha kila kaya ina choo na kuwa na mazingira safi kwa muda wote ili kuutokomeza kabisa ugonjwa huo Wilayani Kyela na kwamba waliokamatwa watafikishwa mahakamani kujibu tuhuma zinazowakabili.


Mtendaji wa Kijiji cha Lusungo Fadhili Sade amesema kuwa wamefanya ukaguzi katika kaya 681 za kijiji hicho na zote hazina vyoo hali inayofanya mapambano ya kipindupindu kuwa magumu mno kwani wengi wao wamekuwa wakiamini ugonjwa huo unatokana na ushirikina.


Aidha Mtendaji wa Kata ya Lusungo Stephen John amesema wamekuwa wakipokea vitisho kutoka kwa Diwani wa Kata na Mwenyekiti wa kijiji kuwa aache kutangaza kuwa Kata hiyo inakabiliwa na ugonjwa wa kipindupindu kwani ndiyo kunachochea kuongezeka kwa ugonjwa huo ambao unatokana na ushikina na si uchafu au ukosefu wa vyoo.
 
Support : Creating Website | Greyson Salufu Template | Chimbuko Letu Inc
Copyright © 2011. Kamanga na Matukio - All Rights Reserved
Template Modify by Chimbuko Letu Inc
Proudly powered by Blogger