Pages


Home » » MWEKEZAJI WA KAPUNGA AZIDI KUWA MWIBA KWA WAKAZI WA KAPUNGA - MBARALI MBEYA.

MWEKEZAJI WA KAPUNGA AZIDI KUWA MWIBA KWA WAKAZI WA KAPUNGA - MBARALI MBEYA.

Kamanga na Matukio | 07:06 | 0 comments
Meneja uzalishaji wa Kapunga Rice Project Bwana SERGEI BEKKER akielezea ramani ya Mashamba ya Kapunga.
******
Habari na Ezekiel Kamanga, Mbarali.(Picha zaidi tembelea mtandao huu).
 Mwekezaji wa shamba la Mpunga la Kapunga Rice Project amezidi kuwanyanyasa wananchi wa Kijiji cha Kapunga wilaya ya Mbarali mkoani Mbeya kwa vitendo mbalimbali vya kikatili, vikiwemo kuwapiga viboko wananchi kwa kutumia fimbo, kuwachoma sehemu za miili yao kwa kutumia waya za umeme, kuua mifugo yao kwa kuwagonga na gari na kisha kufunga barabara zinazoingia na kutoka kijijini hapo kuelekea mashambani.

Mwishoni mwa Mwaka uliopita Mkuu wa mkoa wa Mbeya Mheshimiwa Abbasi Kandoro alimkanya katika kikao mwekezaji huyo na kumtaka asiwanyanyase wananchi mpaka pale Serikali itakapofanyia ufumbuzi suala la mipaka ya shamba hilo na kijiji cha Kapunga.

Kinara wa manyanyaso hayo ni Kaburu anayejulikana kwa jina la Gerry Baquzein (46), ambaye mapema mwaka uliopita alimgonga mkazi wa kijiji hicho aitwaye Mwigulu Ngulu kwa kutumia gari kama digidigi na kulazwa katika Hospitali ya Chimala na kisha kuhamishiwa katika Hospitali ya Ifisi wilaya ya Mbeya Vijijini kwa ajili ya matibabu zaidi.

Wakati huohuo inadaiwa Bwana Gerry alimchoma kwa kutumia nyaya za umeme mlinzi mmoja, aliyekuwa akilinda katika Shamba hilo akidai mlinzi huyo ameiba grender. Januari 7, mwaka huu kwa makusudi aliwafukuza wafugaji wawili kwa kutumia gari yake nambari T. 566 BQH aina ya Landcruiser kwa nia ya kuwagonga wafugaji hao ambao ni Mungo Makubi (27) na Singu Mwakami (23), majira ya saa 11 jioni, walipokuwa wakichunga ng'ombe wa Makubi Dundo (52).

Vijana hao walisalimika baada ya kukimbia katika mti ndipo hasira za Bwana Gerry ziliishia kumgonga ng'ombe mmoja jike aliyekuwa akinyonyesha, na baadae ng'ombe huyo mwenye thamani ya shilingi laki 6 kufa.

Tukio hilo liliripotiwa kwa Mwenyekiti wa Kitongoji Bwana Sangalali Mashishanga ambaye naye alitoa taarifa kwa Mwenyekiti wa Kijiji Bwana Ramadhani Nyoni ambaye alitoa taarifa kituo cha polisi wilaya ya Mbarali.

Mkuu wa kituo cha Polisi wilaya hiyo alifika eneo la tukio na kushuhudia ukatili huo na kudai kuwa suala hilo lipo juu ya uwezo wake, na kwamba Bwana Gerry alikiri kutenda kosa hilo na kueleza kuwa wafugaji huingiza mifugo katika shamba hilo.

Kwa upande wake Kamanda wa Polisi mkoa wa Mbeya Advocate Nyombi amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kwamba Jeshi la polisi linafanya uchunguzi na endapo Bwana Gerry atabainika kutenda makosa hayo atafikishwa kwenye vyombo vya sheria ili kujibu tuhuma zinazo mkabili.

Hata hivyo Mkuu wa wilaya ya Mbarali Kanali Cosmas Kayombo amepata taarifa ya tukio hilo na kwamba atalifikisha katika kamati ya ulinzi na usalama mkoa wa Mbeya inayotarajiwa kukutana Januari 10, mwaka huu.
Share this article :

0 comments:

 
Support : Creating Website | Greyson Salufu Template | Chimbuko Letu Inc
Copyright © 2011. Kamanga na Matukio - All Rights Reserved
Template Modify by Chimbuko Letu Inc
Proudly powered by Blogger