Pages


Home » » Viongozi wa waendesha pikipiki waachia ngazi baada ya kutuhumiwa kufuja fedha za Chama hicho Shilingi Milioni 15.

Viongozi wa waendesha pikipiki waachia ngazi baada ya kutuhumiwa kufuja fedha za Chama hicho Shilingi Milioni 15.

Kamanga na Matukio | 02:58 | 0 comments
Na Ezekiel Kamanga, Mbeya.
Viongozi wa Chama cha Waendesha Pikipiki (BODABODA) Jiji la Mbeya wamelazimika kuachia ngazi baada ya kutuhumiwa kufuja fedha za Chama hicho Shilingi Milioni 15(15,000,000/=) zilizokuwa zikikusanywa na viongozi hao kwa kipindi cha miaka minne.
 Hayo yalibainishwa juzi katika Mkutano uliofanyika kwenye ukumbi wa Tumaini ulioko Ilomba Jijini Mbeya ambao uliwakutanisha Viongozi wa Vituo vya Bodaboda vya Uyole, Kabwe, Soweto, Mafiati, Mwanjelwa, Ilomba, Sai na Stendi kuu.
Wakizungumza katika kikao hicho viongozi wa Mpito wa Chama hicho chini ya Mwenyekiti Jackson Nusurupia aliwaambia wajumbe wa Mkutano huo kuwa fedha zilizofujwa ni pamoja na viingilio vya wanachama Shilingi Milion Sita, Fedha za Ushirika Shilingi 855,000/=, Vitambulisho Shilingi 545,000/=, Fedha za tozo na adhabu kwa waendesha bodaboda wanaobeba abiria zaidi ya Mmoja(mishikaki) Shilingi Milion 7.1/= pamoja na Fedha zilizotolewa na Naibu Waziri wa Elimu Philipo Mulugo Shilingi Laki tano na kufanya jumla ya Milion 15.
Mwenyekiti huyo alisema kufuatia tuhuma hizo viongozi hao walijiuzulu wao wenyewe ili kupisha uchunguzi, ambapo Uongozi wa muda ulichaguliwa ili kuendelea kuendesha chama hicho hadi Mei 20, Mwaka huu uchaguzi mkuu utakapofanyika.
Alisema baada ya kujiuzulu kwa uongozi huo Wanachama waliwachagua viongozi wa Muda ambao ni Jackson Nusurupia (Mwenyekiti), Eliudi Clemens (Makamu Mwenyekiti), Msumba Mdesa( katibu) pamoja na wajumbe watano ambao ni Mishael Mwashilindi, Elly Bariki, Wilson Bukuku, Noah John na Ayubu Mwaisakila.
Aliwataja watuhumiwa wa kesi hiyo kuwa  ni Vicent Mwashoma aliyekuwa Mwenyekiti, Fred Mwambene (makamu Mwenyekiti), Yonah Mwaipungu(katibu) na John Bosco aliyekuwa Mtunza hazina wa Chama hicho.
Nusurupia alisema Viongozi hao hawakuwahi kutoa taarifa ya mapato na matumizi tangu kuanzishwa kwa Chama chao Mwaka 2009 na kuongeza kuwa baada ya kutuhumiwa walitakiwa kukabidhi nyaraka zote za Chama pamoja na kuhudhuria Mkutano lakini hawajafanya hivyo jambo linaloashiria kuhusika na Ubadhilifu huo.
Kwa upande wake Viongozi wanaotuhumiwa walijitetea kuwa habari za kuliwa Fedha si za kweli kwa sababu Chama kina Jumla ya Shilingi 589,000/= na kwamba fedha zilizotolewa na Naibu Waziri zimetumika na kubakia Shilingi 185,000/=na kusisitiza kuwa taarifa zote zipo na zitatolewa kwenye mkutano mkuu.
Mwenyekiti aliyejiuzulu wadhifa wake huo alisema Fedha za viingilio za wanachama hazijawahi kukusanywa kwa kile alichodai kuwa Wanachama walikuwa wabishi wa kuchangia, na kuongeza kuwa fedha za adhabu zilirudishwa kwenye vituo vya Bodaboda kwa Wenyeviti huku zingine zikiwa zimelipiwa faini Polisi kwa wenye makosa.
Mkutano huo uliosimamiwa na Walezi wa Chama hicho ambao ni Jeremia Magacha na Isack Jackson Lema ambao ni Maofisa wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya, walisema hawapingani na maamuzi ya viongozi ambapo waliwasihi wanachama kuwa watulivu katika kipindi cha mpito wakati wakisubiri taarifa za uchunguzi na kuongeza kuwa baada ya kubainika Sheria itachukua mkondo wake ambapo Mkutano uliahirishwa hadi Mei 20, Mwaka huu utakapofanyika Mkutano mkuu.
Share this article :

0 comments:

 
Support : Creating Website | Greyson Salufu Template | Chimbuko Letu Inc
Copyright © 2011. Kamanga na Matukio - All Rights Reserved
Template Modify by Chimbuko Letu Inc
Proudly powered by Blogger