Pages


Home » » SHITAMBALA AITAHADHARISHA JAMII KUHUSU SIASA ZA UCHOCHOZI

SHITAMBALA AITAHADHARISHA JAMII KUHUSU SIASA ZA UCHOCHOZI

Kamanga na Matukio | 03:11 | 0 comments
KULIA NI CAPT.SAMBWEE SHITAMBALA WAKATI ANARUDI CCM AKIKUMBATIANA NA RAIS JAKAYA KIKWETE (Picha Maktaba).

NA SOLOMON MWANSELE,KYELA

MJUMBE wa halmashauri Kuu ya Taifa (NEC), ya CCM, Sambwee Shitambala, amesema watanzania hawana utamaduni wa kuvipenda vyama vyenye lengo la kutaka kuigawa nchi katika vipande.

Imeelezwa wakati CCM imekuwa kila mara ikiongelea umoja na mshikamano miongoni mwa watanzania, CHADEMA wao wanataka kuigawa nchi kwa kuanzisha mfumo wa majimbo.

Shitambala aliyasema hayo jana wakati akihutubia mamia ya wananchi wa wilaya ya Kyela, waliojitokeza katika maadhimisho ya miaka 36 ya kuzaliwa kwa Chama Cha Mapinduzi (CCM), wilayani humo.

Alisema uhuru, umoja na mshikamano ndiyo misingi ya CCM, tofauti na CHADEMA ambao mara zote wao wamekuwa mabingwa ya kuwahamasisha na kuwashawishi wananchi kuandamana, kuchoma barabara na kufanya vurugu zisizo na msingi.

“Tunahitaji kuendelea kuwa na Tanzania moja, lakini wenzetu wa CHADEMA wao wanataka kuigawa nchi katika majimbo.Watanzania hatupendi vyama vyenye lengo la kuigawa nchi yetu kimajimbo” alisema Shitambala na kushangiliwa.

Aliongeza CCM kupitia serikali zake, kimeleta maendeleo mengi na yanayoonekana wazi kwa watanzania, hivyo kuwataka wananchi wa wilaya ya Kyela na watanzania kwa jumla, kuwapuuza wanaaiasa wanaosema hakuna lililofanyika tangu nchi ipate uhuru 1961.   

Mjumbe huyo wa NEC alisema hakuna serikali yoyote duniani, inayoweza kuwajaza wananchi wake fedha mifukoni, hivyo kutoa rai kwa wana-Kyela wawe makini na kamwe wasikubali kuchuuzwa na wanasiasa uchwara.

Alisema CCM imekuwa inasimamia vyema ugawaji na usimamizi makini wa rasilimali za Taifa letu, tofauti na CHADEMA ambao wao kupitia sera yao ya majimbo, wanataka kila mkoa unufaike na rasilimali zake badala ya Taifa zima.

Shitambala alisema vile vile CCM imekuwa na demokrasia ya kweli kwa viongozi wake kuchaguliwa kwa kura na wananchi, tofauti na CHADEMA ambao wamekuwa wanagawana uongozi kwa kutanguliza undugu, urafiki na ukabila.

“Mimi sijawahi kuwa mpinzani bali nilienda CHADEMA kuangalia jinsi wanavyoendesha siasa zao kwa kutanguliza ukabila… napenda kuitumikia nchi yangu, ndiyo maana nilipoona wanataka kunitumia kuendesha mikutano ya vurugu niliwakimbi na kurudi CCM” alisema Shitambala.

Aliongeza CCM kinataka watu wachape kazi kwa bidii na maarifa kwa lengo a kuinua vipato vyao na ndiyo maana licha ya sikukuu ya kuzaliwa kwake (Februali 5, ya kila mwaka), iliangukia siku za kazi, lakini kwa busara za hali ya juu kiliamua kurudisha nyuma sherehe zake.

Shitambala alisema CCM haikudondoka kama Uyoga kama vilivyo vyama vingine vya siasa nchini, na ndiyo maana vyama vingine havina waasisisi kama ilivyo kwa CCM ambayo ni zao la TANU na Afro Shiraz.
Share this article :

0 comments:

 
Support : Creating Website | Greyson Salufu Template | Chimbuko Letu Inc
Copyright © 2011. Kamanga na Matukio - All Rights Reserved
Template Modify by Chimbuko Letu Inc
Proudly powered by Blogger