Pages


Home » » WASUSIA KUZIKA MAITI KWA SIKU MBILI,MFIWA ATAKIWA KULIPA SHILINGI 460,000/= ILI APEWE MSAADA..

WASUSIA KUZIKA MAITI KWA SIKU MBILI,MFIWA ATAKIWA KULIPA SHILINGI 460,000/= ILI APEWE MSAADA..

Kamanga na Matukio | 05:34 | 0 comments
Habari na Ezekiel Kamanga,Mbozi.
Wananchi wa Kitongoji cha Njiapanda,Kijiji cha Msamba,Kata ya Nyimbili,Wilaya ya Mbozi Mkoani Mbeya,walisusa kuzika maiti kwa takribani siku mbili na nusu kwa kile kilichodaiwa kuwa mfiwa alikuwa hahudhurii misiba wenzie kijijini hapo.

Hayo yalibainishwa na mwandishi wa habari hii baada ya kufika kijijini hapo,ambapo imedaiwa Bwana Samson Mwazembe(35),ambaye alifiwa na mwanae aitwaye Hassan Samson(7) mwanafunzi wa darasa la kwanza Shule ya Msingi Chizumbi wilayani humo,aliyefariki siku ya Ijumaa Septemba 7 mwaka huu majira ya saa 10 alfajiri.

Mtoto huyo anadaiwa kufariki baada ya kuugua ugonjwa wa kuharisha kwa muda wa siku tatu lakini hakufanikiwa kupelekwa hospitali kwa ajili ya matibabu.

Baada ya kifo hicho,kutokana na kasumba ya Bwana Mwazembe kutohudhuria katika misiba kijiji hapo,aliamua kwenda kutoa taarifa katika Kituo cha Polisi cha wilaya hiyo ili kuomba msaada wa kusaidiwa kuzika mwanae,lakini polisi walikataa na kumtaka arudi kijijini ili azungumze na wananchi.

Kufuatia juhudi zake kugonga ukuta,aliamua kujifungia ndani ya nyumba yake na ndipo mkewe aitwaye Bi.Daina Kananda(25),aliamua kwenda kumuona Mwenyekiti wa kitongoji Bwana Eston Silomba ambapo alikwenda kwa Mwenyekiti wa Kijiji Bwana Ikson Halihoka Sikaponda(48) kwa pamoja walimtaka mfiwa azike mwenyewe kutokana na tabia yake ya kutohudhuria misibani.

Aidha,baada ya agizo hilo Bwana Mwazembe wakati akielekea tena katika Kituo cha Polisi alikutana na kaka njia aitwaye Bwana Adam Mwazembe(55),na alimwambia warudi kijijini na kuchukua jukumu la kuomba msamaha kwa uongozi wa kijiji ili wamsamehe mdogo wake huyo,viongozi walikataa ombi hilo na kumtaka mfiwa alipe jumla ya shilingi 460,000 ikiwa shilingi 400,000 kwa ajili ya kuchimba kaburi na shilingi 60,000 ya jeneza la kumhifadhia marehemu.

Hata hivyo mfiwa alikataa kulipa akidai kuwa hana fedha zozote ndipo maiti ikabaki bila kuzikwa na asubuhi ya Jumamosi Septemba 8 mwaka huu,Bwana Mwazembe alifanikiwa kupata shilingi 110,000 nakuomba uongozi upokee fedha hizo lakini bado walikataa na kumweleza kuwa akachimbe kaburi mwenyewe na kukabidhiwa vifaa vya kuchimbia lakini alishindwa na kubaki akiangua kilio.

Septemba 9,mwaka huu siku ya Jumapili ndugu wa Bwana Mwazembe kwa pamoja walimueleza auze mifugo wakiwemo mbuzi,nguruwe vilevile mazao(mahindi) baada ya kuuza jumla ya shilingi 400,000 zilipatikana lakini wananchi waliendelea kuwa na msimamo wakitaka zitimie shilingi 460,000,ndipo Mwandishi wa habari hii alipowasihi wananchi wakubali kupokea pesa hizo walikubali na kufanya mazishi majira ya saa 8 mchana.

Uchunguzi umebaini kuwa mfiwa anatuhumiwa kujihusisha na imani za kishirikina kwani mkewe alishawahi kujifungua watoto wawili na baadae kufariki kwa nyakati tofauti na yeye kuwazika pasipo kutoa taarifa kijijini na baadhi ya viungo kuvichukua na kuvipeleka kusikojulikana.

Wakati huohuo Bwana Mwazembe,amedai sababu za kutohudhuria katika misiba ni kutokana na kusisikia utofauti awapo msibani na ndiyo sababu ambayo hupelekea kutohudhuria.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa kijiji Bwana Sikaponda amesema kuwa hilo ni fundisho kwa mfiwa huyo na kwamba asirudie tena kitendo hicho na kwamba kijiji hakitatoa msamaha tena bali watamtaka kuondoka kijijini hapo kutokana na kutokuwa na ushirikiano.

Katika pesa zilizotolewa na mfiwa Bwana Mwazembe,shilingi 50 ilitumika kununulia vifaa vya kuchimbia kaburi kijijini hapo.

(Picha zaidi za tukio hili fuatilia mtandao huu)
Share this article :

0 comments:

 
Support : Creating Website | Greyson Salufu Template | Chimbuko Letu Inc
Copyright © 2011. Kamanga na Matukio - All Rights Reserved
Template Modify by Chimbuko Letu Inc
Proudly powered by Blogger