Pages


Home » » MAKALA

MAKALA

Kamanga na Matukio | 05:33 | 0 comments
Na Gabriel Mbwille
Katika maisha yaliyo ya kawaida tunafahamu kuwa kifo kinapotokea huwa kimepangwa na Mwenyezi Mungu, lakini pia kwa wakati mwingine kifo husababishwa bila ridhaa ya mwenyezi Mungu, na ndio maana kunakuwa na vyombo vya kisheria dhidi ya watu waliosababisha vifo katika tawala mbalimbali zikiwemo za kimila, kidemokrasi na hata zile za kidikteta.

Katika vifo ambavyo kila mmoja anaamini kuwa kimepangwa na Mwenyezi ni pamoja na kifo cha mtu kinachotokana na maradhi mbalimbali ama ajali, lakini inapotokea mtu akafariki dunia kwa kupigwa ama kuchinjwa na mtu mwingine jamii huamini kuwa kifo hicho si mpango wa Mungu na ndio maana watu ama mtu anayehusika na kifo hicho hukamatwa na kufikishwa kwenye vyombo vya dola ili sheria iweze kuchukuwa mkondo wake.

Hata hivyo kutokana na utaratibu huo bado jamii imekuwa ikijiuliza maswali mengi kuhusu hatua na maamuzi yanayotolewa na vyombo vya dola dhidi ya watu wanaohusika kwa namna moja ama nyingine na matukio ya mauaji hapa nchini hasa zaidi wakiwemo vigogo wa  nchi na askari polisi wanaonekana kulindwa zaidi kuliko raia wa kawaida.

Duniani kote, mara nyingi wahusika wa mauaji ya kisiasa ndio hubahatika kufutiwa adhabu na kurejea uraiani. Adhabu ya kosa la kuua kwa kukusudia ni kunyongwa hadi kufa. Mkuu wa nchi ndiye hutia saini kuidhinisha mtu aliyehukumiwa kifo anyongwe, japo kutokana na kampeni ya asasi zinazopigania kufutwa adhabu ya kifo, hukumu ya kifo imekuwa ikibatilishwa na kuwa kifungo cha maisha jela.

Ibara ya 15 (1) (c) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 ilivyofanyiwa marejeo mwaka 2005 inamruhusu Rais kutoa msamaha.

Ibara hiyo inatamka “Bila kuathiri masharti mengineyo yaliyomo katika Ibara hii, Rais anaweza kutenda lolote ikiwamo kuibadilisha adhabu yoyote aliyopewa mtu yeyote kwa kosa lolote ili iwe adhabu tahafifu.”

Kama adhabu ya kuua kwa kukusudia inasameheka, kwa nini Rais asiwasamehe mamia ya ‘wauaji’ walioko magerezani kwa maana wameadhibiwa vya kutosha? Kama adhabu ya kuua kwa kukusudia inasameheka, kwa nini Rais asiwasamehe wenye vifungo virefu vya makosa tena siyo ya kuua kama Nguza Viking na mtoto wake Papii Nguza?

Ushahidi uliotolewa wakati wa kesi hiyo ulionesha wazi Koplo Mswa na konstebo Matiku walimuua Jenerali Kombe kwa kumpiga risasi baada ya kudhani kwamba alikuwa mtuhumiwa sugu wa uhalifu.

Polisi hao walimkimbiza Jenerali Kombe aliyekuwa na mkewe. Alipoona hatari Jenerali Kombe alinyanyua juu mikono kujisalimisha, lakini bado wauaji wakamimina risasi kifuani na kumuua.

Mauaji hayo yalifanyika katikati ya uvumi kwamba Jenerali Kombe alikuwa akikisaidia chama cha upinzani cha NCCR-Mageuzi ambacho mwenyekiti wake alikuwa Augustine Lyatonga Mrema.

Hicho ndiyo kipindi ambacho Mrema alikuwa akilipua mabomu akifichua mipango, mikakati na njama za serikali kuua upinzani.

Mazingira haya ndiyo yaliwafanya watu wahisi kwamba mauaji ya Jenerali Kombe yalikuwa ya kisiasa. Ilihisiwa kwamba polisi hao hawawezi kusota jela miaka mingi kwa vile walitumwa. Miaka 16 tangu Jenerali Kombe auawe mazingira yanathibitisha hisia za watu – mauaji ya kisiasa!

Kwa nini wanaonufaika ni wanasiasa tu? Mwaka 1969  na 1983 wanasiasa na wanajeshi waliokamatwa kwa tuhuma za kutaka kuipindua serikali ya Mwalimu Nyerere wote waliachiwa huru baada ya mifumo ya kisiasa waliyopigania kubadilika.

Waliokamatwa kwa tuhuma za uhaini mwaka 1969 ni pamoja na Bibi Titi Mohammed, Waziri wa Kazi, Michael Kamaliza. Walihukumiwa kifungo cha maisha jela lakini wakasamehewa mwaka 1972.

Mwaka 1983 vijana kadhaa wakiwemo kepteni Eugene Maganga, Suleiman Kamando, Zakaria Hanspop, Vitalis Mapunda, Mbogolo, Kajaji Badru, Hatty MacGhee na Christopher Kadego walikamatwa na wakatiwa hatiani mwaka 1985 kwa kula njama kutaka kumpindua Nyerere.

Watuhumiwa hao walipewa kifungo cha maisha jela lakini baada ya kuanzishwa mfumo wa vyama vingi mwaka 1991 waliachiwa huru mwaka 1995.

Juhudi za serikali kubatilisha adhabu ya kifo zilionekana kwa aliyekuwa mkuu wa mkoa wa Tabora, Ukiwaona Ditopile Mzuzuri. Mkuu wa mkoa huyo alichukua bastola yake akaelekeza kwa dereva wa daladala, Hassan Mbonde akafyatua na kumuua katika njiapanda ya Kawe na Bagamoyo.

Kortini wakasema Ditopile (sasa marehemu) ameua bila kukusudia kosa ambalo mtuhumiwa anaweza kusamehewa au kupewa kifungo cha miaka kadhaa. Halafu akapewa dhamana.

Koplo Mswa na Konstebo Matiku wako huru baada ya Mr Clean kutumia madaraka aliyopewa kwa mujibu wa Katiba. Vema.

Lakini huenda ukajiuliza maswali mengi sana je wafungwa wengine wa maisha wanapaswa kutimiza vigezo gani ili wafikiriwe kusamehewa? Wawe maarufu? Wawe na ndugu wanaojua sheria? Wawe viongozi kama vile Ditopile? Wawe polisi? Ndiyo wawe polisi maana hata polisi 13 waliofanya njama na kuua kwa makusudi wafanyabiashara watatu wa madini kutoka Mahenge na dereva teksi mmoja mwaka 2006 waliachiwa huru eti kwa kukosa ushahidi. Kikatiba si watu wote sawa mbele ya sheria?
Machi 2009 Deus Mallya alifunguliwa kesi ya kusababisha ajali iliyoua mjini Dodoma na akafungwa jela miaka mitatu baada ya kupatikana na hatia.

Kwanza ni kwa kuendesha gari kwa uzembe, pili ni kusababisha kifo cha aliyekuwa Mbunge wa Tarime, Chacha Wangwe, na tatu kuendesha gari bila leseni. Mallya hakupewa dhamana.

Mahakama ya Wilaya ya Singida, ilimhukumu dereva wa basi la kampuni ya Adventure ya jijini Mwanza, Robert Willison (37), kifungo cha miaka 153 na miezi sita jela baada ya kupatikana na makosa 49 tofauti likiwamo la kusababisha vifo vya watu tisa mwaka 2008.

Robert alisomewa mashitaka matatu: la kwanza lilikuwa na makosa tisa ya kusababisha vifo vya watu tisa; la pili makosa 36 ya kusababisha watu 36 kujeruhiwa na shitaka la tatu lilikuwa na kosa moja la kuendesha basi bila leseni kutoka mkoani Kigoma kwenda Dar es Salaam.

Lakini mahakama hiyohiyo ilimwachia huru dereva wa basi la kampuni ya Mohamed Trans ya jijini Mwanza, Kharabu Jordan (43) ambaye alikabiliwa na shitaka la kusababisha ajali iliyoteketeza abiria 25 kwa moto na kujeruhi wengine kadhaa.

Mahakama ilidai ushahidi uliotolewa na upande wa mashitaka dhidi ya Jordan ulikuwa dhaifu.
Katika kesi nyingine ya kigogo wa Serikali Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Kinondoni-Kivukoni, Kwey Rusema alimtia hatiani aliyekuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Andrew Chenge na kumhukumu kifungo cha miaka mitatu jela au kulipa faini ya Sh. 700,000.

Makosa yaliyosababisha Chenge, ambaye awali alishitakiwa kwa mauaji na baadaye kubadilishiwa mashitaka yakawa, atiwe hatiani ni kuendesha gari kwa uzembe, kusababisha ajali iliyowaua Beatrice Constantine na Victoria George, kuharibu mali na kuendesha gari lisilo na bima. Hakimu alithibitisha kuwa Chenge alighushi bima.

Tofauti na Mallya au dereva wa Mohamed Trans, Chenge ambaye ni Mbunge wa Bariadi Magharibi na mwenyekiti wa nidhamu wa CCM, alipewa fursa ya kulipa faini ya Sh. 700,000 hivyo akakwepa kifungo cha miaka mitatu jela.

Kushiriki katika uhalifu au kushiriki kupanga njama za kufanya uhalifu, polisi wanasema ni kosa la jinai na mhusika anaweza kutiwa jela.

Lakini Jaji aliyesikiliza kesi ya kuuawa wafanyabiashara watatu wa Mahenge, mkoani Morogoro, na dereva teksi mmoja mwaka 2006, alisema katika hukumu yake kwamba aliyeua hajulikani, akawaachia polisi wote walioshiriki.

Katika tukio hilo, wapo polisi walikiri kubeba vijana wale na kuwapeleka msitu wa Pande walikouliwa, wapo walioshuhudia bunduki ikifyatuliwa, wapo waliochukua maiti kupeleka Muhimbili – jaji hakuona ushiriki wao isipokuwa alitaka aliyeua.

Utetezi mkubwa wa wataalamu wa sheria ni kwamba watu wengi hawazijui sheria. Je, hiyo ndiyo sababu ya kuwakomoa walalahoi kwa adhabu kali kwa kosa ambalo mjuzi wa sheria anaachiwa huru?
Ukweli tatizo si wananchi kutojua sheria zilizopo, bali ni kukosekana uadilifu, ujuzi makini, utashi wa majaji na mahakimu na kukithiri kwa rushwa kunakosababisha mahakimu na majaji kutumia vifungu batili au kutoa tafsiri iliyopinda ili kuwaridhisha mafisadi.

Hata mashtaka huandaliwa katika namna ya kukandamiza walalahoi na kuwaokoa wakubwa.
Aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Ukiwaona Ramadhani Ditopile Mzuzuri, baada ya gari lake kugongwa na basi la abiria (DCM) alishuka, akatoa bastola na kumtwanga risasi dereva na kumuua.

Polisi wa serikali wakafika kusoma hali, wakafikiria jinsi ya kumwokoa, wakapima na kuandika ripoti.
Ripoti ikasomeka Ditopile aligongwa, akashuka kwenye gari lake kwa bahati mbaya, akachukua bastola kwa bahati mbaya, akamgongea dirisha dereva wa DCM kwa bahati mbaya, akamlenga na kumuua kwa bahati mbaya.

Mkurugenzi Mkuu wa Mashtaka (DPP) aliposoma akafungua kesi ya kuua bila kukusudia, na akapewa dhamana. 

September 02, 2012 majira ya saa 10 za jioni mwandishi wa habari mwandamizi wa kituo cha Chanel Ten mkoani Iringa Daudi Mwangosi aliuawa kikatili na chakushangaza ni jinsi, jeshi la polisi mkoani Iringa kutaka kuuficha ukweli kuhusu kifo hicho na kutoa taarifa za awali kuwa, marehemu Mwangosi alifariki dunia baada ya kupigwa na kitu kizito ambacho kilirushwa na kutoka kwa wafuasi na viongozi wa Chadema.

Hata hivyo wakati akitoa jibu hilo hakuwa na ufahamu kuwa wakati akiongea Watanzania wote walikuwa wamekwisha fahamu kilichotendeka maeneo hayo ya Nyololo wilayani Mafinga kwa kupitia njia ya mitandao ya kijamii baada ya moja ya wanahabari kupiga picha na kuziweka kwenye mitandao hiyo.

Kutokana na maeneo hayo ya kamanda wa polisi wa mkoa wa Iringa kuhusu taarifa za kwamba marehemu aliuawa kwa kupigwa na kitu kizito kutoka kwa wafuasi wa CHADEMA je kamanda alikuwa na lengo gani hapo?Kila mtu anaweza kujiuliza anavyoweza lakini ninachoweza kusema kuwa huenda Taifa likaingia kwenye mvutano mkubwa na vyombo vya usalama kutokana na vyombo hivyo kutoa kauli zake zenye utata mara kwa mara.

Pia tunaweza kujiuliza maswali mengi je ni kwanini basi mtuhumiwa wa mauaji ya Mwangosi hakuweza kuchukuliwa hatua za haraka, na kwanini hatua ilichukuliwa baada ya wananhabari hapa nchini kufanya maandamano ya kulaani vikali mauaji hayo.Pia kunamasawali ambayo nadhani kila mtu huenda akawa anajiuliza kuhusu kifo hicho na haki je itaweza kutendeka kwasababu siku ya ambayo mtuhumiwa anafikishwa mahakamani alipelekwa huku akiwa  kwenye gari la kifahari, la Land Cruiser, polisi kuzuia kabisa, mtuhumiwa huyo, asipigwe picha na paparazi. 

Vile vile, kitendo cha Kamuhanda kutoshtakiwa na kuendelea na kazi, wakati inafahamika wazi kuwa yeye, ndiye aliyesimamia hiyo operesheni ya mauaji ya Mwangosi unafikiri inaleta picha gani kwa watanzia ambao hivi wanaouelewa mkubwa wa waya yanayoendelea hapa nchini?

Hata hivyo kutokana na tukio hilo waandishi mbalimbali mkoani Iringa wamekuwa wakiwinda na baadhi ya watu wanaodhaniwa kuwa ni askari na kutishiwa kuuawa hali iliyowalazimu baadhi yao kuamua kuandika ushahidi wao kwa maandishi na kuuweka pia katika sauti ushahidi utakao saidia mahakama kutenda haki wakati wa kutoa hukumu ya kesi hiyo.

Pamoja na hayo bado kuna wasiwasi mkubwa wa haki kutendeka baada ya hivi karibuni KAMATI iliyoundwa na Waziri wa Mambo ya Ndani, Dk. Emmanuel Nchimbi kwa ajili ya kuchunguza mauaji ya mwandishi wa habari, marehemu Daudi Mwangosi, kutukana na baadhi ya wajumbe wa kamati hiyo wakiwa mkoani Iringa kuibiwa Ipad iliyokuwa na nyaraka muhimu za uchunguzi wa tukio hilo.

Baadhi ya wajumbe hao waliibiwa fedha na vifaa vya kazi vyenye thamani ya mamilioni ya fedha kwenye hoteli waliyofikia, muda mfupi baada ya kuwasili mjini hapa.

Wajumbe walioibiwa katika tukio hilo ni pamoja na Theophil Makunga ambaye ameibiwa ipad, kamera na fedha taslimu zaidi ya sh milioni moja.

Mwingine ni Mwenyekiti wa kamati hiyo, Jaji Stephen Ihema ambaye naye ameibiwa zaidi ya sh milioni moja na mjumbe mwingine ameibiwa sh 150,000.

Pamoja na hayo kamati hiyo ilionekana kuwa na hofu kubwa kutokana na mazingira ya wizi na jinsi walivyoibiwa katika hoteli hiyo ya Ruaha International.

Inaelezwa kwamba baada ya kuwasili na kupumzika kidogo katika vyumba vyao, walipanga kwenda kupata chakula cha jioni.

Wakiwa nje wakisuburi chakula, mtu mmoja ambaye hajanaswa na polisi, kwa kutumia funguo maalumu alifungua kwenye vyumba vya wajumbe hao na kuiba fedha na vifaa hivyo.

Wadadisi wa mambo ya siasa wanahoji kuwa ni kwa vipi mwizi huyo aliweza kufungua vyumba hivyo tu na kuacha vingine.

Hoja ya msingi inayoweka njia panda wajumbe wa kamati hiyo ni juu ya usalama, kwamba mwizi huyo ameweza kuingia kwenye vyumba vyao bila kukamatwa, ni kwa vipi wanaweza kuwa na uhakika wa usalama wao?

Mmoja wa wafanyakazi wa hoteli hiyo aliliambia gazeti moja la kila siku kuwa ni mara ya kwanza kwa wizi wa aina hiyo kutokea hotelini hapo.

“Nina muda mrefu hapa hotelini, sijaona wizi wa aina hii. Nadhani mwizi huyo aliwafuatilia sana wajumbe na alijipanga,” alisema mfanyakazi huyo.

Hata hivyo hadi sasa hakuna aliyekamatwa kuhusika na tukio hilo na polisi wanaendelea na uchunguzi.
Wajumbe wengine wanaounda kamati hiyo ni Mwakilishi wa Baraza la Habari Tanzania (MCT), Pili Mtambalike, mtaalamu wa milipuko kutoka Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), Kanali Wema Wapo na Naibu Kamishna wa Polisi (DCP), Isaya Mngulu.

Wajumbe hao wamepewa hadidu rejea yenye maswali sita ambayo ni kujua chanzo cha kifo cha Mwangosi, iwapo kuna uhasama kati ya polisi na waandishi Iringa na kama kweli kuna orodha ya waandishi watatu wa kushughulikiwa mkoani Iringa.

Swali lingine ni kama nguvu zilizotumika zilistahili, kama kuna utaratibu wa vyama vya siasa kukata rufaa dhidi ya uamuzi wa polisi na kujua uhusiano wa Jeshi la Polisi na vyama vya siasa ukoje.

Katika hatua nyinyine, hofu ya kutaka kumtorosha askari, Pasificus Cleophace Simon, anayetuhumiwa kwa mauaji ya aliyekuwa mwandishi wa habari wa Kituo cha Televisheni cha Channel Ten, Daudi Mwangosi.
Mbinu za kutaka kumtorosha askari huyo, namba G2573, zinadaiwa kufanywa na baadhi ya askari wenzake wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU) kwa kushirikiana na baadhi ya maofisa wa Polisi wanaodai kutoridhishwa na hatua ya kupandishwa kizimbani kwa askari huyo pekee.

Mkakati wa askari waliozuia kwa kuwasukuma waandishi wa habari wasimpige picha mtuhumiwa, huku akijifunika kitambaa usoni inatajwa kuwa moja ya mbinu iliyopangwa ili mtuhumiwa asijulikane machoni kwa watu.

Siku moja baada ya askari huyo kupandishwa kizimbani, kulikuwa na mazungumzo ya baadhi ya askari wa FFU waliokuwa katika ukumbi wa baa moja uliopo ndani ya jengo la Iringa Net jirani na Benki ya Posta wakielezea mpango huo.

Askari hao wanne, waliokuwa wamevalia kiraia, katika mazungumzo yao walitoboa siri kubwa ya kumnusuru askari mwenzao kwa kumtorosha nje ya nchi, vinginevyo kesi hiyo itamuelemea.
Walisema kuwa wamejaribu kwa kila njia kufikiria jinsi ya kumnasua mwenzao, mwisho wakakubaliana afikishwe mahakamani ili asomewe mashitaka yake kama kawaida, huku wakifanya mpango wa kumkimbiza nje ya nchi halafu baada ya kufanikisha wataiambia mahakama mtuhumiwa ametoroka.

Wakati hayo yakizungumzwa ndani ya baa hiyo, mmoja wao alisema Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP), Said Mwema, asingekubali askari huyo afikishwe mahakamani na kuendelea kusota mahabusu, kwani wangekuwa tayari kulipuana ili kuhakikisha mkuu huyo wa Jeshi la Polisi na viongozi wengine wa Polisi, wanakuwa miongoni mwa watuhumiwa.

“IGP Mwema alitumia busara kufanya hivyo vinginevyo kule ndani kusingekalika. Ungekuwa ni uonezi mkubwa kama mwenzetu atiwe gerezani wakati alikuwa akitii amri yao wenyewe.

“Inabidi ifanyike haraka iwezekanavyo ili hata Kamanda Kamuhanda aondoke maana wananchi wameshapata hasira, usione wamekaa kimya ipo siku lolote linaweza kutokea,” alisema mmoja wao.
Tuliongea na Mwema siku mbili ikaonekana Kamuhanda hawezi kukwepa kesi hiyo. Hivyo tumepanga kumkimbizia nje ya nchi,” alisema mmoja wa askari polisi mkoani humo.

“Hii kesi ina watu wengi na isingekuwa hii mbinu inayotaka kutumika kumtorosha mtuhumiwa, Kamuhanda na wengine wasingepona kwa sababu yule kijana hatakubali kutumikia jela peke yake wakati haukuwa uamuzi wake.

“Tulipanga kwamba wakati mtuhumiwa anafikishwa mahakamani askari watakaomsindikiza wahakikishe wanamlinda kwa kila njia ili asipigwe picha akajulikana sana, kwani akijulikana hata huko atakakopelekwa anaweza kukamatwa tena. Si uliona jinsi askari walivyofanya mahakamani kuzuia asipigwe picha?” kilisema chanzo chetu cha habari.

Ilielezwa kuwa tayari mtuhumiwa huyo ametengenezewa cheti kingine cha kuzaliwa chenye jina la Kacian Alphonce Mapila, huku akielezwa kuwa ni Mhehe tofauti na kabila lake (Mhaya).

Kwa maelezo hayo kila mtu anaweza kuwa na fikra tofauti kuhusu ukweli wa kesi hiyo na kuona namna ambavyo jeshi limekuwa likitumia kila njia kulindana ili kukwepa aibu ya chombo hicho muhimu cha kusimamia usalama wa raia na mali zake baada ya wao kuwa chanzo cha kupoteza maisha ya raia na uhalibifu wa mali za mwananchi.

Kwa kesi hiyo huenda watu wakawa na mawazo hasi kwa wanahabari kuwa wanataka kulikandamiza jeshi la polisi kwa kuwa mwenzao kauwa lakini vipi kuhusu vifo vingine vya raia vinavyotokana na kupigwa na polisi, Mbeya mwanafunzi wa shule ya sekondari Iyunga aliuawa mikononi mwa polisi, kwenye vurugu za Mwanjelwa tumeona watu zaidi ya 6 wakijeruhiwa kwa kupigwa risasi na polisi, vurugu za Tunduma raia mmoja aliuawa naye ambapo baadaye ilitoelewa taarifa kuwa alikuwa akijaribu kuiba benki jambo ambalo si kweli na hivi karibuni mwanachama wa CHADEMA aliuawa mkoani Morogoro.

Kutokana na hayo je haki itaweza kutendeka kweli?Vipi kuhusu maamuzi yanayotolewa na viongozi, wanahabari na raia usalama wao uko wapi kunapotekea mikutano ya kisiasa, na kwanini viongozi wa kuu wa wameshindwa kuzungumzia hilo?
Kwa maoni 0714-558777.
Share this article :

0 comments:

 
Support : Creating Website | Greyson Salufu Template | Chimbuko Letu Inc
Copyright © 2011. Kamanga na Matukio - All Rights Reserved
Template Modify by Chimbuko Letu Inc
Proudly powered by Blogger