Pages


Home » » UHABA WA WALIMU WA MASOMO YA SAYANSI,SERIKALI YASHAURIWA KUANDAA MIKAKATI ENDELEVU JUU YA VIJANA

UHABA WA WALIMU WA MASOMO YA SAYANSI,SERIKALI YASHAURIWA KUANDAA MIKAKATI ENDELEVU JUU YA VIJANA

Kamanga na Matukio | 02:40 | 0 comments
Na Bosco Nyambege,Mbeya
Serikali imeshauriwa kuwa na mikakati maalumu ya kuwaandaa Vijana katika misingi ya kuyapenda masomo ya Sayansi kwa lengo la kuwa walimu watakaobobea katika ufundishaji wa masomo hayo yatakayowasaidia wanafunzi kujitegemea na siyo kutegemea ajira.

Wito huo umetolewa na baadhi ya wakuu wa shule za sekondari mkoani Mbeya wakati wa mahojiano maalum kuhusiana na uhaba wa walimu wa sayansi mashuleni na kitu ambacho kinapelekea kukosa walimu wa masomo hayo.

Kwa upande wake mwalimu mkuu wa Shule ya sekondari Regco iliyopo Jijini Mbeya,Joshua Mwakitalima amesema kuwa ili kujenga kizazi ambacho kitaweza kujitegemea na kupambana na maisha ni vema Serikali ikajikita zaidi katika kuzalisha walimu vijana ambao pia watafundishwa mbinu za kuwawezesha wanafunzi pindi watakapohitimu wajue jinsi ya kujitegemea.

Ameongeza kuwa katika masomo yafundishwayo mashuleni, ni masomo ya Sayansi pekee ndiyo yanaweza kumjengea msingi wa kujitegemea mwanafunzi pindi amalizapo masomo yake bila kutegemea ajira.
  
Aidha ameongeza kuwa hivi sasa Serikali ni kama inaelekea kuua masomo ya sayansi kwa sababu wahitimu wengi ni masomo ya Art na kufanya idadi kubwa ya walimu mashuleni kuwa wa masomo hayo tofauti na walimu wa Sayansi.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Jiji la Mbeya, Juma Iddi ambaye ndiye mwajiri mkuu wa Halmashauri ya Jiji alipohojiwa kuhusu tatizo hilo alikiri kuwepo na kuongeza kuwa hilo ni janga la kitaifa.

Iddi amesema upungufu wa walimu wa sayansi limechangiwa sana na ongezeko la shule nyingi za kata hivyo serikali imeshindwa kuendana na kasi hiyo katika kuleta walimu wa sayansi ambao hata vyuoni ni wachache.

Ameongeza kuwa Jiji la Mbeya linahitaji jumla ya walimu 412 kwa shule zote lakini badala yake kuna walimu 215 hivyo kuwa na upungufu wa walimu 197 ambapo amesema ni upungufu mkubwa na tatizo hilo linatakiwa lipewe kipaumbele.

Aliongeza kuwa tatizo lingine linalosababisha upungufu wa walimu wa sayansi ni kuwahamisha baadhi ya walimu wenye digrii kuwapeleka katika shule zingine ili hali wenye diploma ni wachache na hawajitoshelezi.

Ametanabaisha kuwa Halmashauri ya Jiji ina mpango wa kuongeza walimu wa sayansi katika Mwaka wa fedha wa Mwaka 2012-2013 ambapo katika bajeti yao wanatarajia kupata walimu 86 ambao pia hawataziba pengo la upungufu huo kwa kuwa bado kuna shule zinaongezeka.
Share this article :

0 comments:

 
Support : Creating Website | Greyson Salufu Template | Chimbuko Letu Inc
Copyright © 2011. Kamanga na Matukio - All Rights Reserved
Template Modify by Chimbuko Letu Inc
Proudly powered by Blogger