Pages


Home » » KIKWETE ATEKELEZA AHADI YA UMEME ILEMBO.

KIKWETE ATEKELEZA AHADI YA UMEME ILEMBO.

Kamanga na Matukio | 02:48 | 0 comments
Na Ezekiel Kamanga, Mbeya..
RAISI wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. Jakaya Mrisho Kikwete ametekeleza ahadi ya kuwawekea umeme wakazi wa kijiji cha Ilembo Wilaya ya Mbeya Mkoani hapa.
 
 
Ahadi hiyo iliahidiwa na Raisi katika kampeni ya Uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 baada ya kupita kijijini hapo na kukuta nguzo za umeme zikiwa zimesimikwa na kutelekezwa bila kuendelezwa kwa muda wa miaka 8.
 
 
Umeme huo uliowashwa mwezi uliopita umeonekana kuwafurahisha wakazi hao ambao bila kificho walimpongeza raisi kwa kutekeleza ahadi hiyo ya umeme na kufanya kijiji hicho kusahaulika kwa muda mrefu.
 
 
Akizungumza na waandishi wa habari kijijini hapo Mwenyekiti wa kijiji hicho Abeli Amon mbali na kutoa pongezi kwa raisi kutokana na kutekeleza ahadi hiyo pia ametoa wito kwa Shirika la Umeme Tanesco kusambaza nguzo nyingi kutokana na mwitikio wa wananchi kuhitaji nishati hiyo.
 
 
Mwenyekiti huyo alisema kutokana na uwepo wa nishati hiyo shughuli za kiuchumi zimeongezeka kwa kasi kubwa kutokana na wananchi kutumia nishati hiyo kuzalisha na kufanya shughuli za kimaendeleo.
 
 
Alisema shirika la Umeme Tanesco ni vema likapeleka miundombinu ya umeme katika kila kaya kijijini hapo kutokana na utayari wa wananchi ambao walikuwa na hamu kubwa ya kuona umeme ukiwaka kijijini hapo.
 
 
Alisema miaka nane ni mingi sana tangu Tanesco wasimike nguzo lakini walishindwa kuendeleza hadi hapo alipofika raisi na kusikia kilio chao na hatimaye kuwatekelezea ahadi hiyo na kuwatimizia ahadi ya umeme.
 
 
Nao baadhi ya wananchi walioongea na gazeti hili,wameiomba Wizara ya Afya kupitia Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya kuingiza umeme katika kituo cha afya cha Ilembo ili usaidie katika kurahisisha huduma.
 
 
" Wizara husika ni vema ikaingiza umeme katika kituo cha afya ili kusaidia katika huduma za upasuaji na wakati wa kujifungua kwa akina mama" alisema Shizya Halinga mkazi wa kijiji hicho.
 
 
Naye Benard Shusa alisema uwepo wa umeme utasaidia uhifadhi wa mazingira kwa wananchi kuacha kukata miti ovyo kwa ajili ya nishati na badala yake watatumia umeme kwa kazi mbali mbali.
 
 
Aliongeza kuwa wananchi walikuwa wakiharibu mazingira kutokana na kukata miti ambayo walikuwa wakitumia kuchoma mkaa na shughuli zingine kama za kupikia ambapo sasa wanaweza kununua majiko ya umeme ili kurahisisha huduma hiyo.

Share this article :

0 comments:

 
Support : Creating Website | Greyson Salufu Template | Chimbuko Letu Inc
Copyright © 2011. Kamanga na Matukio - All Rights Reserved
Template Modify by Chimbuko Letu Inc
Proudly powered by Blogger