Pages


Home » » Mama Pinda awashukia mafataki

Mama Pinda awashukia mafataki

Kamanga na Matukio | 04:56 | 0 comments
·         Ataka watoto wa kike wapewe kipaumbele katika elimu
·         Ni wale wanao walaghai wanafunzi

Mke wa Waziri Mkuu wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama Tunu Pinda, amewakemea baadhi ya wanaume wanaotumia matatizo waliyonayo wanafunzi wa kike na kuwalaghai ili watimize haja zao kwa kuwarubuni kuwahudumia huku akiitaka jamii ya Watanzania kuwapa watoto wa kike kipaumbele katika elimu.
Mama pinda ameyasema hayo katika uzinduzi wa mradi wa Msichana kwanza uliofanyika mkoani Mtwara huku akitanabaisha kuwa watoto wengi wa kike wanashindwa kuhudhuria masomo pale wanapokuwa kwenye hedhi.
Alisema, hali hiyo inatokana na ukweli kwamba wasichana wanaotoka kwenye familia zinazoishi katika hali duni hukosa haki ya kimsingi ya kuweza kumudu usafi wao na kushindwa kuhudhuria masomo yao huku akiwakemea wanaume “Mafataki” wanaowalaghai mabinti kwa kuwahaidi kuwahudumia.
“Baadhi ya wasichana, kwa kukosa mahitaji muhimu zikiwemo pedi, wamejiingiza katika mahusiano ya kimapenzi na ’mafataki’ ambao huwaahidi kushugulikia mahitaji yao. Hali hii haikubaliki”
“Tatizo la hedhi limekuwa likiwasumbua mabinti wetu hasa walioko katika maeneo ya vijijini na wengine walioko katika mazingira duni, alisema Mama pinda.
Mradi huo ambao umeandaliwa na TMARC na USAID kwa ufadhili wa Vodacom Foundation umelenga kuwakomboa wasichana wanaokosa kuhudhuria masomo mashuleni wakati  wakiwa kwenye hedhi umelenga kuwa endelevu na wa gharama nafuu kwa kuwawezesha wasicha zaidi ya 10,535 waliopo ndani na nje ya shule kwa kuanzia mikoa ya Lindi na Mtwara.
Pamoja na kuishukuru Vodacom, T -MARC na USAID, Mama Pinda ameongeza kuwa ni vyema sasa jamii ikaliona tatizo hilo na kulipa kipaumbele haina haja ya kufumbia macho tatizo hili ili kuwawezesha watoto wa kike kutimiza malengo yao na ndoto zao huku akitoa wito kwa viongozi wa serikali hasa katika ngazi za mikoa kuhakikisha mradi huo unafanikiwa na kuwa endelevu kwa kutoa ushirikiano unaofaa kwa wahusika na kuhakikisha waalimu wanahusishwa kwa ukaribu zaidi.
Nae Mkuu wa Kitengo cha Huduma za Jamii (Vodacom Foundation), Yessaya Mwakifulefule, alisema kuwa “Tunaamini kwamba mradi huu utabadilisha tabia na hivyo kupunguza tabia hatarishi za ngono miongoni mwa vijana sambamba na kujikinga na kuanza kushiriki ngono mapema kama njia ya kupunguza mimba kwa wasicha wadogo mashuleni, kuepusha maambukizi ya magonjwa yanayoambukiza kama vile UKIMWI na pia kupunguza utoro mashuleni.” 
Aidha, Mwakifulefule alisema kuwa baada ya kipindi cha miaka miwili, mradi huo unapaswa kutoa mafunzo ya jinsi ya kujitunza na kufanya usafi na hivyo kuwapatia manufaa endelevu na stahiki kwa jamii katika mikoa hiyo ya Lindi na Mtwara.
“Tunaamini kwamba mradi huu utafika mbali katika suala zima la usafi kwa wasichana mashuleni sambamba na kudumisha heshima yao binafsi,” alisema Mwakifulefule, akiongeza kuwa, “Vodacom Foundation imewekeza kiasi cha shilingi milioni 160.”
Kwa upande wake Mkurugenzi wa T - MARC Diana kisaka, alisema kuwa mradi huo wa majaribio wa miaka miwili unalenga kuwafikia mabinti wote wanaoishi katika mazingira duni.
“Lengo la mradi huu ni kuwasaidia wasichana hawa ambao wamekuwa hawaudhurii masomo kwa sababu ya kushindwa kumudu gharama za mataulo maalum kwa ajili kuwasitiri wakati wanapokuwa kwenye hedhi kitu ambacho kimechangia kufanya vibaya mashuleni. Hivyo, tunaamini kwa kuanzisha mradi huu utawasaidia kuboresha mahudhurio yao mashuleni sambamba na matokeo yao kuwa mazuri,” alisema Kisaka.
Share this article :

0 comments:

 
Support : Creating Website | Greyson Salufu Template | Chimbuko Letu Inc
Copyright © 2011. Kamanga na Matukio - All Rights Reserved
Template Modify by Chimbuko Letu Inc
Proudly powered by Blogger